Tuesday, May 3, 2016

Shahidi Kesi Ya Askofu Gwajima Aeleza Jinsi Begi Lilivyokutwa Na Silaha

SHAHIDI, Pamphilly Mholeli, katika kesi inayomkabili Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima na wenzake ya kukutwa na silaha kinyume cha sheria, amedai mahakamani kwamba, siku ya tukio aliwakamata mshtakiwa pili hadi wa nne wakiwa na begi lenye silaha wakati askofu huyo akiwa chini ya ulinzi wa polisi.

Amedai kabla ya kulikagua begi walitilia mashaka ujio wa mshtakiwa wa pili hadi wa nne nje ya wodi namba 113 ya hospitali ya TMJ, jijini Dar es Salaam saa 9:00 alfajiri wakati Askofu Gwajima alipokuwa amelazwa huku akiwa chini ya ulinzi wa polisi na baada ya kulikagua begi walilokuwa wamebeba walikuta bastola moja, risasi 17 na vitu vingine.

Ushahidi huo ulitolewa jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Mfawidhi, Cyprian Mkeha, anayesikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.

Akiongozwa na mawakili wa serikali waandamizi, Shadrack Kimaro na Jackline Nyantori, shahidi huyo alidai kuwa, siku ya tukio akikuwa ofisa wa polisi wa zamu kwa mkoa wa kipolisi Kinondoni, usiku wa manane alipokea agizo kutoka kwa bosi wake Costantine Masare kwamba kuna kundi kubwa la watu limekusanyika katika Hospitali ya TMJ.

“Nilikwenda eneo la tukio na tuliwatawa wale watu, lakini tulipoikwenda kuangalia lindo la polisi nje ya wodi namba 113 ghorofa ya kwanza aliyokuwa amelazwa Gwajima, tuliwakuta washtakiwa pamoja na askari aliyekuwa akilinda, nilipowauliza washtakiwa wanahitaji nini muda ule na begi lao, walijieleza kwamba walikwenda kumuona mgonjwa”alidai na kuongeza:

“Nilishangaa saa 9:00 alfajiri walikuwa wanakwenda kumuona mgonjwa gani, nililitilia shaka lile begi nikawakamata na kuwaweka chini ya ulinzi, baada ya kulikagua ndani lilikuwa na bastola moja, risasi 17 pamoja na vitu vingine, tukashangaa kwanini walikuja na silaha wakati askofu yuko kwenye mikono salama ya Jeshi la Polisi” alidai Mholeli.

Shahidi huyo aliomba mahakama ipokee hati yenye orodha ya vitu vilivyokutwa kwenye begi hilo baada ya kupekuliwa na ombi hilo lilikubaliwa na kupokelewa kielelezo.

Kesi hiyo ilitajwa Mei 2, mwaka huu ilipopangwa tarehe ya kuendelea kusikilizwa na dhamana ya washtakiwa inaendelea.

Mbali na Gwajima wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo ni Askofu Msaidizi wa kanisa hilo, George Mzava, Mfanyabiashara Yekonia Bihagaze na Mchungaji Georgey Milulu, wote wanakabiliwa na mashitaka ya kukutwa na bastola bila kibali.
Share:
Weka Maoni yako Hapa

Habari Zinginezo:

0 comments:

Post a Comment

Become a Fan

Popular Posts

Copyright © 2025 GUMZO LA JIJI | Powered by Blogger