Showing posts with label burudani. Show all posts
Showing posts with label burudani. Show all posts

Monday, April 18, 2016

Ofisi ya Bunge Yalivaa Gazeti la Nipashe....!



Ofisi ya Bunge imebaini upotoshwaji mkubwa Katika habari iliyochapishwa na Gazeti la Nipashe toleo la Aprili 16, 2016 yenye kichwa cha habari kisemacho “ Bunge sasa laufyata mkataba wa Lugumi”. 
Habari hiyo imeandikwa kufuatia ufafanuzi uliotolewa na Bunge jana kuhusu maagizo yaliyotolewa na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) dhidi ya utekelezaji wa mkataba wa Jeshi la Polisi na Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd  kuhusu mradi wa utambuzi wa alama za vidole (AFIS) (Automated Fingerprint Identification System.)
 
Ndani ya habari hiyo pia, Gazeti hilo limeeleza kuwa kamati ya PAC iliwahi kuliandikia Jeshi la Polisi kulitaka liwasilishe mkataba huo mbele ya Kamati, jambo ambalo si kweli bali ni upotoshwaji wa makusudi wenye lengo la kujenga hisia mbaya kuhusu mwenendo wa shughuli za Bunge mbele ya Umma.
 
Ukweli ni kwamba PAC haijawahi kuliandikia jeshi la Polisi kama inavyodaiwa na Gazeti hilo. Nukuu ya  maelezo ya PAC katika Hansard kwa Afisa Masuhuli kuhusu jambo hilo inasema kama ifuatavyo:
 
“Kamati inamuagiza Afisa Masuhuli kuwasilisha maelezo ya kina kuhusu utekelezaji wa Mkataba baina ya Jeshi la Polisi na  Kampuni ya Lugumi Enterprises  kuhusu mradi wa AFIS. Maelezo hayo yawasilishwe kwa Ofisi ya  Katibu wa Bunge kabla ya Jumatatu tarehe 11 Aprili, 2016”.
 
Katika agizo hilo PAC haikuwa imeandika kwa maandishi kuhusu agizo lake hilo hadi tarehe 12 Aprili, 2016 ilipo mweleza Katibu wa Bunge aweze kuwasilisha agizo hilo kwa maandishi ili liweze kupata Kinga chini ya Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge ambapo barua iliandikwa na kuwasilishwa kwa Afisa Masuhuli ili kupatiwa maelezo hayo kabla ya tarehe 18 Aprili, 2016.

Aidha, Mwandishi pia amelituhumu Bunge kuwa lina nia ya kuficha ukweli kuhusu jambo hili kwa kusema   taarifa ya ufafanuzi iliyotolewa na Bunge ni “kama kufunika kombe mwanaharamu apite kwa kujaribu kupotosha maagizo ya yaliyotolewa na kamati ya PAC ambayo inataka kuuona mkataba huo”

Ni vyema ikafahamika kuwa si jambo jema kwa mwandishi au chombo chochote cha habari kulituhumu Bunge linapotekeleza majukumu yake kwa kuwa Bunge linafanya kazi zake kwa kwa kuzingatia kanuni zake za Kudumu ikiwa ni pamoja na Sheria.  
 
Ofisi ya Bunge inalisihi Gazeti la Nipashe kuomba radhi kutokana na taarifa yake hiyo iliyojaa upotoshwaji mkubwa kwa uzito ule ule au kurekebisha taarifa yake kulingana na ukweli ulivyo haraka iwezekanavyo.

Imetolewa na;
Ofisi ya Bunge,
Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano,
S.L.P 9133,
DAR ES SALAAM.
16 Aprili, 216
Share:

Waziri Mkuu Aiambia DART, Hakuna Muda Wa Kulala

 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewaambia watendaji na wadau wa mradi Mabasi Yaendayo Haraka wa jijini Dar es Salaam (BRT) kuwa hawana muda wa kulala kupumzika na akawataka wakamilishe haraka vipengele vichache vilivyobakia ili mradi huo uweze kuanza kazi mapema iwezekanavyo.

Ametoa agizo hilo juzi usiku (Ijumaa, Aprili 15, 2016) wakati akizungumza na wakuu wa taaasisi, watendaji wakuu na wadau wa mradi huo kwenye kikao alichokiitisha ofisini kwake Magogoni jijini Dar es Salaam.

“Watu wa DART, UDA-RT hakuna muda wa kulala tena. Nanyi wa eGA, MAXCOM, POLISI NA SUMATRA inabidi mfanye kazi kama timu moja na wenzenu ili maeneo yaliyobakia yaweze kukamilika katika muda mfupi na kikubwa ni kuhakikisha mnatoa elimu ya kutosha,” alisisitiza.

Akielezea utekelezaji wa agizo la Waziri Mkuu, Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), Bw. Ronald Rwakatare amesema miundombinu ya mradi huo imekamilika na utoaji huduma unatarajiwa kuanza hivi karibuni kwani hivi sasa wanamalizia ufungaji wa mfumo wa ukusanyaji nauli na uendeshaji wa mabasi hayo.

Pia aliwataka wananchi kutunza miundombinu ya mradi huo na kuwa makini na matumizi ya barabara wakati mradi huo ukiwa kwenye majaribio na hatimaye kuanza kazi rasmi.

Alisema watakuwa na karakana itakayotumika kwa ajili ya hayo mabasi ambayo itakuwepo eneo la Jangwani na kwamba ofisi za mradi pia zitakuwa eneo hilo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa UDA Rapid Transit (UDA-RT), Bw. Robert Kisena amesema mpango wa kuanza kwa mradi huo umekamilika na tayari mabasi yote yamelipiwa kodi pamoja na bima. UDA-RT ni kampuni ya muunganiko wa UDA na wamiliki wa daladala ya kutoa huduma ya usafiri katika miundombinu ya mabasi yaendayo haraka.

Bw. Kisena amesema leo wataanza majaribio ya mradi huo kwa kutumia mabasi 10 na watakuwa wanaongeza mabasi 10 kila siku hadi yafikie 50 hivyo amewataka wananchi kuondoa shaka juu ya mradi huo.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Maxcom Africa, Bw. Juma Rajab amesema mabasi hayo yatakuwa yanatumia kadi za kielektroniki zitakazokuwa zinalipiwa kwa kutumia mitandao mbalimbali ya simu za mkononi.

Bw. Rajab amesema Tanzania inakuwa nchi ya kwanza kuanza kutumia mfumo huo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na kwamba fedha za mteja zitakuwa salama na hata kama atakapopoteza kadi yake.

“Mtu akinunua kadi yake anapaswa atunze namba ya usajili iliyoko kwenye kadi hiyo kwani itatumika kurudishia fedha zake kupitia namba yake ya simu ya mkononi,” alisema.

Amesema Maxcom Africa ndio wakusanyaji wa nauli kwa kushirikiana na UDA-RT ambapo watatumia mawakala wa MaxMalipo hivyo kila mwananchi atapata fursa ya kununua kadi yake kwa urahisi.

Alisema taarifa za kila mtumiaji zitaunganishwa na simu yake ya mkononi ambapo mhusika ataweza kujua kwa urahisi salio la fedha lililomo kwenye kadi yake.
Share:

Paul Makonda: Baadhi ya Ombaomba Wanauza Madawa ya Kulevya


Mkuu  wa Mkoa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema kwa mujibu wa utafiti alioufanya, ombaomba walioko jijini Dar es Salaam baadhi yao wanajihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya.
Akihojiwa katika mahojiano ya moja kwa moja na kituo kimoja cha redio, Makonda alisema wapo watu ambao wanatumia mwanya huo kusambaza dawa za kulevya.

“Wapo wanaotumia fursa hii kusambaza dawa za kulevya kwa sababu anavyopita huwezi kumhisi kwa namna anavyoonekana, lakini watu hawa ni miongoni mwa mawakala wa kusambaza dawa za kulevya,” alisema Makonda.

Makonda aliwataka wakazi wa jiji hilo kushirikiana naye katika kuwaondoa ombaomba hao ambao wengi wanatoka nje ya Da es Salaam na kwamba hakuna tija kuendelea kuwaacha. 

“Watanzania tuna upendo sana lakini tunahitaji kutafakari kama kweli watu walioko barabarani wakiomba kama kweli wanahitaji msaada huo au la,” alisema Makonda.

Alisema kwa kuendelea kuwaacha ombaomba hao pia kutasababisha vijana ambao sasa wanaomba barabarani kuwa watu hatari katika maisha yao ya baadaye kwani wakikosa pesa wataingia katika shughuli za uporaji ili wapate fedha.

“Itafika kipindi ataanza kuangalia kile alichokuwa anakikusanya wakati akiomba na kile anachokipata akifanya kazi, ataona akifanya kazi hapati kiasi kikubwa, ataamua kuwa mporaji,alisema Makonda.

Makonda alisema kwa mujibu wa utafiti alioufanya, asilimia 80 ya ombaomba wanatoka nje ya Dar es Salaam na kesho operesheni ya kuwaondoa watu hao itaanza rasmi huku wale ambao hawana ulemavu wowote wakikamatwa kwa makosa ya uzururaji.
Share:

Rais Magufuli Awataka Mawaziri wasioweza Kazi Bila Posho au Safari Wajiondoe Wenyewe

 
Viongozi  serikalini wakiwemo mawaziri na makatibu wakuu, wameombwa na Rais John Magufuli, kuvumilia machungu wakati wa uongozi wake, kama ambavyo wananchi walivyovumilia tangu Uhuru.

Amesema hayo jana wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya kwanza ya juu (flyover) nchini Tanzania, inayojengwa katika makutano ya Barabara ya Mandela na Barabara ya Nyerere, eneo la Tazara, kwa ufadhili wa Serikali ya Japan. 
Machungu hayo kwa mujibu wa Rais Magufuli, yataanza kuonekana wakati wa utekelezaji wa Bajeti ya Serikali ya kwanza kwa Awamu ya Tano, ambayo fedha za maendeleo zimeongezeka kutoka asilimia 27 za bajeti iliyopita, hadi kufikia asilimia 40.

Machungu yenyewe 
Ili kufanikisha dhamira hiyo ya Serikali, Rais Magufuli alisema katika bajeti hiyo inayotarajiwa kupelekwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, litakaloanza vikao vyake Dodoma wiki ijayo, machungu hayo yataanza kuonekana kwani fedha za chai, semina na safari, zimekatwa na kujaziwa katika fedha za maendeleo.

Kutokana na makato hayo, Dk Magufuli amesema kutakuwa na machungu hasa kwa watendaji wa Serikali na kuwaomba mawaziri na makatibu wakuu ambao alisema walikuwa wakifaidi matunda ya Uhuru, wavumilie machungu hayo kwani wananchi wa maisha ya chini wamevumilia machungu kwa muda mrefu.

“Wananchi wamechoka kutuona sisi viongozi tunafaidi matunda ya Uhuru wa nchi tangu Uhuru na wao wakiwa wasindikizaji halafu wao tunawaomba kura na wakishatupigia tunawasahau,” alisema na kuongeza kuwa anataka wananchi watoke kwenye machungu na sasa wawe ‘watamu’ kwa maendeleo.

Magufuli alisema lazima viongozi wabadilike na kurudi kwa wananchi wa maisha ya chini na hiyo itakuwa sadaka kwa kuwapa madaraka kwani wananchi wanyonge wameteseka siku nyingi.

Wasiovumilia 
Alisema waliokuwa wamezoea chai, safari na posho za ovyo kama wanaona au wanafikiri hawawezi kufanya kazi bila hizo chai, waache kazi mara moja kwani sasa fedha zinazokusanywa za walipa kodi wanyonge, zitaenda kutatua matatizo yao ya hospitali, barabara na kununua ndege za Serikali.

Pia alionya kuwa katika uongozi wake hakuna mtu atakayekwenda kinyume na utaratibu na kisha ‘akachomoka salama’ na kama kuna anayeona hawezi ajiondoe mwenyewe kwani Watanzania wanaendelea kumuombea.

Dk Magufuli alisema wananchi wote bila kujali vyama vya siasa, wanalilia maendeleo na maendeleo hayana chama, kwani wananchi wamechoka ‘machama chama’, wanataka kwenda mbele, hivyo hakuna sababu ya kubaki nyuma na kubishana kwa mambo ya chama chama, wakati uchaguzi umepita na aliyeshinda ni yeye ambaye ni CCM.

Machungu ya zamani 
Ingawa Rais Magufuli alisema machungu hayo yataanza kuonekana katika Bajeti inayotarajiwa kuanza kujadiliwa na Bunge litakaloanza vikao wiki ijayo, lakini watendaji wa Serikali walianza kuona machungu ya msimamo wake tangu alipoingia madarakani Novemba mwaka jana.

Itakumbukwa kuwa Novemba 7, mwaka jana akiwa Ikulu, Dar es Salaam, katika mkutano wake wa kwanza na watumishi wa ngazi za juu wa Serikali, hasa makatibu wakuu, naibu makatibu wakuu na watendaji wengine wakuu wa Serikali, Rais Magufuli alitangaza kufuta safari zote za nje ya nchi hadi hapo atakapolitolea suala hilo uamuzi mwingine.

Mpaka sasa Rais Magufuli amehakikisha shughuli zote zinazotakiwa kufanywa nje ya nchi zinafanywa na kusimamiwa na mabalozi wa Tanzania wanaowakilisha nchi, ambapo watumishi watasafiri nje iwapo kutatokea jambo la dharura na pamoja na udharura wake, lazima kibali kitolewe na yeye, Katibu Mkuu Kiongozi au Makamu wa Rais.

Katika kile kinachoonekana kuwa hatanii, Rais Magufuli aliagiza kusimamishwa kazi mara moja kwa watumishi waandamizi wanne wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ambao walikaidi agizo lake la kuwataka watumishi wa umma kutosafiri nje ya nchi.

Watumishi hao ni Mary Mosha, Ekwabi Mujungu, Doreen Kapwani na Rukia Nikitas ambao walisafiri kwenda nje ya nchi, licha ya kutokuwa na kibali cha safari kutoka kwa Rais ama Katibu Mkuu Kiongozi.

Aidha ndani ya siku zake 100 za kwanza tangu alipoingia madarakani, tayari Serikali yake ilikuwa imeshawafukuza kazi vigogo zaidi ya 70 kwa tuhuma mbalimbali ikiwamo za ufisadi.

Novemba 9, mwaka jana, aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Sefue, alitangaza kuwa Rais Magufuli aliamua kufuta shamrashamra za Sikukuu ya Uhuru ambapo fedha zilizookolewa aliagiza zipelekwe katika mradi wa kupanua kipande cha barabara kutoka Morocco mpaka Mwenge katika wilaya ya Kinondoni.

Hatua hiyo ilitanguliwa na kupunguza fedha za sherehe ya kupongezana ya wabunge, ambazo alizielekeza kwenda kununua vitanda, magodoro na mashuka kwa ajili ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Hivi karibuni alipokuwa akiapisha wakuu wa mikoa, aliwataka kwenda kuwasaka watumishi hewa na kutangaza idadi yao, ambapo aliyeteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anne Kilango Malecela, aliposema hajakuta watumishi hewa wakati wapo, Dk Magufuli hakusita kumuondoa mwanzoni mwa wiki hii, ingawa hakuwa amemaliza hata mwezi tangu aripoti kazini.
Share:

Become a Fan

Popular Posts

Copyright © GUMZO LA JIJI | Powered by Blogger