Tuesday, July 21, 2015

Kafulila aendelea kukomaa na Escrow, atoa siri nyingine

MBUNGE wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), ametoa siri ya moyoni kwamba kashfa ya sakata la fedha za Akaunti ya Tegeta Escrow lilimkutanisha na Makamu wa Rais Dk. Mohammed Gharib Bilali ili kumueleza ukweli wa sakata hilo.

Vilevile, amesema Dk. Bilal ndiye kiongozi pekee wa Serikali ambaye alionesha dhahiri kuwa aliguswa kutokana na wizi huo wa fedha za umma.Kafulila alisema hayo wakati akipokea tuzo ya Mtanzania mwenye maono mapevu iliyotolewa juzi na Taasisi ya Dream Success Enterprises, jijini Dar es Salaam.
Alisema ametoa siri hiyo sasa kutokana na ukweli kuwa kiongozi huyo wa pili kwa madaraka nchini kumuita na kufanya mahojiano naye kwa saa nne kuanzia saa nne usiku hadi saa nane ili kumueleza kuhusu sakata hilo hiyo ikiwa ni baada ya kupotoshwa na watendaji wa Serikali.

Mbunge huyo alisema, baada ya kuitwa alipata wasiwasi mkubwa kwani haijawahi kutokea, akalazimika kuwataarifu ndugu zake kuwa ameitwa na makamu wa rais hivyo asiporejea wajue kwamba aliitwa na kiongozi huyo.

Kafulila alisema baada ya kufika makamu wa rais alitaka kujua nini kipo katika sakata hilo hiyo ikiwa ni baada ya viongozi wanapokutana na mataifa yaliyoendelea, wahisani na mashirika ya fedha wanashindwa kuelewana hali ambayo ilichangiwa na upotoshaji wa watendaji.
Alisema alipofika alimueleza kila kitu kuhusu sakata hilo la Escrow ndipo Dk Bilal akapata ufahamu na kukiri kuwa alikuwa anadanganywa na watendaji wake hivyo kupatwa na huzuni kubwa kwa kuongea uongo mbele ya wahisani ambao walikuwa wanajua kila kitu.

“Katika sakata la Escrow kuna jambo ambalo sijawahi kulisema leo (juzi) nasema kwa sababu naona watu waadilifu hawathaminiwi, nakumbuka siku moja saa nne usiku niliitwa na Makamu wa Rais Dk. Bilal hadi sa nane ambapo alitaka nimueleze kila kitu ninachokijua kuhusu Escrow ili aweze kujieleza mbele ya watu mbalimbali jambo ambalo hakuna kiongozi mwingine wa Serikali alifanya hivyo.

“Nilikuwa na taarifa yenye takribani kurasa 600 nilitumia saa nne kumueleza kila jambo, ambapo kimsingi alionekana kuumia sana na aliniuliza hivi kweli rais anajua haya au na yeye yupo kama mimi huku akitikisa kichwa,” alisema Kafulila.

Mbunge huyo alisema kilichoonekana ni wazi kuwa watendaji wa Serikali waliamua kumdanganya au nao walikuwa hawajua jambo ambalo lilimsukuma kutaka kujua ukweli ulivyo.
Alisema pamoja na maelezo yote ambayo aliyatoa kwa Makamu wa Rais saa tisa usiku alifuatwa na watu ambao walikuwa na magari matatu wakimtaka asiseme yote ambayo yapo katika taarifa yake kwani mengine ni makubwa na hatari.

Mbunge huyo alisema siku hiyo umeme ulikatika, lakini watu hao walimpigia simu muda wote na kumtaka waonane aligoma ila baadae alikubali pamoja na ukweli kuwa umeme haukuwepo.
Kafulila alisema kutokana na uzalendo huo ambao Dk. Bilal alionesha aliamini kuwa ni mmoja wa Watanzania wazalendo na waadilifu, lakini katika jambo la kushangaza katika mchakato wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kupitisha majina ya wagombea walimkata bila kuingia hata tano bora.
“Kutokana na uadilifu wa yule mzee nilibakiwa na mshangao pale, ambapo CCM kupitia kamati yake ya maadili kumkata sijui wanatumia kigezo gani kuangalia uadilifu,” alisema.

Sakata la Escrow liliibuliwa na Kafulila ndani ya bunge, ambapo baadae lilifikishwa katika Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Hesabu za Serikali (PAC) ambayo ilifanyia uchuguzi na kutoa taarifa iliyosababisha bunge kutoka na maazimio nane ili Serikali itekeleze.
Baadhi ya maazimio hayo ni Serikali kuwawajibisha Harbinder Singh Sethi, James Rugemalira (VIP), Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Waziri wa Nishati na Madini, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania(Tanesco) walihusika kwa namna moja au nyingine katika kufanikisha kufanyika miamala haramu ya fedha za Akaunti ya Escrow ya Tegeta kwenda kwa makampuni ya Pan African Power Solutions Ltd. (PAP), na VIP Engineering & Marketing (VIP).

Pia, azimio lingine lilikuwa ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na usalama viwachukulie hatua stahiki za kisheria, kwa mujibu wa sheria za nchi watu wote waliotajwa na taarifa maalum ya kamati kuhusika na vitendo vyote vya kijinai kuhusiana na miamala ya Akaunti ya Escrow, na watu wengine watakaogundulika kuhusika katika vitendo hivyo vya jinai kufuatia uchunguzi mbali mbali unaoendelea;

Bunge pia liliazimia Waziri wa Nishati na Madini, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Fredirick Werema, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Eliakim Maswi na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco wawajibishwe, kwa kuishauri mamlaka yao ya uteuzi kutengua uteuzi wao;
Aidha azimio lingine la bunge lilikuwa ni Kamati husika za Kudumu za Bunge zichukue hatua za haraka, na kwa vyovyote vile kabla ya Mkutano wa Kumi na Nane wa Bunge, kuwavua nyadhifa zao Wenyeviti tajwa wa Kamati husika za Kudumu za Bunge ambao walikuwa ni Andrew Chenge, William Ngeleja na Victor Mwambalaswa.

Azimio lingine lilikuwa ni kumtaka Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aunde Tume ya Kijaji ya Uchunguzi kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya Jaji Aloysius Mujulizi na Jaji Profesa Eudes Ruhangisa wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Pia, azimio lingine lilikuwa ni mamlaka husika za kifedha na za kiuchunguzi ziitaje Stanbic Bank (Tanzania) Ltd. na benki nyingine yoyote itakayogundulika, kufuatia uchunguzi wa mamlaka za kiuchunguzi, kujihusisha na utakatishaji wa fedha zilizotolewa katika Akaunti ya Escrow, kuwa ni taasisi zenye shaka ya utakatishaji wa fedha haramu (institutions of money laundering concern).
Bunge liliazimia pia, Serikali iandae na kuwasilisha Muswada wa marekebisho ya Sheria iliyoiunda Takukuru kwa lengo la kuanzisha taasisi mahsusi itakayoshughulikia, kupambana na kudhibiti vitendo vya rushwa kubwa, ufisadi na hujuma za uchumi zinazotishia uhai wa taifa kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Aidha Bunge linaazimia kwamba Serikali iangalie uwezekano wa kununua mitambo ya kufua umeme ya IPTL na kuimilikisha kwa Tanesco kwa lengo la kuokoa fedha za Shirika hilo.
Azimio la nane la Bunge ni Serikali itekeleze Azimio husika la Bunge mapema iwezekanavyo na kwa vyovyote vile kabla ya kumalizika kwa Mkutano wa Bunge la Bajeti Serikali iwasilishe taarifa ya utekelezaji wa mapitio ya mikataba ya umeme jambo ambalo halikufanyika na kusababisha Kafulila kuomba muongozo ndani ya bunge kila mara kuhusu lini taarifa hiyo itawasilishwa.

Source: Jamboleo
Share:
Weka Maoni yako Hapa

0 comments:

Post a Comment

Become a Fan

Popular Posts

Copyright © GUMZO LA JIJI | Powered by Blogger