Wednesday, June 15, 2016

Kiki za Kibongo Zinanikumbusha Hadithi Hii ya Zamani

Hapo zamani za kale palikuwepo na familia iliyojumuisha baba, mama na mtoto mmoja wa kike. Mtoto huyo alikuwa mtundu sana na mara nyingi alikuwa akiwaweka wazazi wake roho juu kutokana na michezo yake ya kipuuzi.

Kila siku usiku muda wa kulala unapofika alikuwa na tabia ya kupiga kelele kuwaambia wazazi wake kuwa chumbani kwake kuna joka kubwa limeingia na linataka kummeza. Basi wazazi wake walipokuwa wakisikia kelele hizo walikuwa wakikanyagana kuwahi chumbani kwa mtoto wao kuangalia joka hilo na kumuokoa.

Kila walipokuwa wakifika walimkuta mtoto wao akicheka na kuwatania wazazi wake ‘haoo waone walivyotoa macho, nilikuwa nawatania tu.’ Basi wazazi walikaushia tu kwakuwa ndivyo walivyomlea mtoto wao na hawakuwa tayari kumwadhibu. 

Huo ndio ukawa mchezo wa mtoto huyo, kila siku ‘mamaa, babaa, joka linataka kunimeza.’ Wazazi watakurupuka tena chumbani kwao kwenda kumwangalia mtoto wao na kukuta hakuna nyoka wala nini! Wakati mwingine walijikuta hata wakijeruhi vidole vyao vya miguu kwa kujigonga kwenye samani za ndani wakiwahi kumsaidia binti yao. Mtoto huyo aliendelea kuwafanyia vituko hivyo kwa muda na kwake ikawa ni burudani kweli kweli. 

Siku moja, joka kubwa kweli liliingia ndani ya chumba cha huyo mtoto. Alipiga kelele kama kawaida kuwaita wazazi wake waende kumuokoa. Wazazi wakapuuzia kwasababu walijuwa kuwa ni yale yale, mtoto wao anawachezea tu. 

Mtoto alipiga kelele kuomba msaada asiupate hadi joka lile likamvunjavunja, likammeza na kutokomea mwituni. Kulipokucha wazazi wake walienda chumbani kumwangalia mtoto wao na kugundua ni kweli usiku palikuja joka na kweli lilimmeza mtoto wao. Walilia na kuhuzunika sana.

HADITHI HII INA UHUSIANO GANI NA KIKI ZA KIBONGO?

Katika kutafuta kuongelewa zaidi kwenye TV, redio, blog na kwenye mitandao ya kijamii, wasanii wetu wamekuwa wakitafuta njia nyingi zikiwemo za kuunda matukio yasiyokuwepo. Mambo mengi sana ambayo yamewahi kusemwa au kutendwa na wasanii yalikuja kugundulika kuwa kumbe yalifanywa kwasababu ya kutafuta kiki tu. 

Kwa mimi kama mwandishi, ninapoona kitu na kukikimbilia haraka nikijua kuwa ni habari nzuri itakayowavutia wasomaji wangu na kuamua kuiandika lakini baadaye nakuja kugundua haikuwa kweli, huwa nasosoneka sana. Na mara nyingi hiyo hunifanya nipunguze kabisa imani na msanii huyo. 

Mashabiki pia hufedheheshwa na kiki hizi na wao pia hupunguza kabisa imani na msanii. Matokeo yake, kama yule mtoto aliyewachosha wazazi wake kwa kelele za kumezwa na nyoka ambaye hakuwepo na pindi nyoka wa kweli anapomvamia wazazi wake wakapuuzia, ndivyo ambavyo wasanii wanaoendekeza kiki hizi watajikuta wakishindwa kuaminiwa tena hata kwa matukio makubwa ya kweli yatakayowahusu.

Wapo wasanii pia ambao wamekuwa na tabia za kuongea uongo uongo ili waonekane wana mambo makubwa wanafanya. Wengine huamua kuishi maisha ‘feki’ kujitengenezea ukubwa ambao hawana. 

Mara nyingi njia ya muongo ni fupi, hujikuta wakiumbuka. Wengine pia huwindwa na maneno yao wenyewe ambayo mwisho wa siku hugeuka kuwa jinamizi linalowatesa.

Acha kazi ziongee kwasababu ‘actions speak louder than words.’Ni vyema wasanii wakafikiria kabla ya kuamua kutengeneza kiki ambazo zitawatokea puani siku za usoni.
Share:
Weka Maoni yako Hapa

0 comments:

Post a Comment

Become a Fan

Popular Posts

Copyright © GUMZO LA JIJI | Powered by Blogger