Monday, April 25, 2016

Viongozi wa Chama cha UDP Watimkia CCK

Mwenyekiti wa Taifa wa UDP, John Cheyo

Viongozi wa Chama cha UDP wamekihama chama hicho na kujiunga na Chama cha Kijamii (CCK), kwa madai kinaongozwa kibabe, hakuna mikutano wala vikao vinavyofanyika ili kukijenga.

Viongozi hao ni aliyekuwa mkurugenzi wa uchaguzi wa UDP na Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Mtwara, Salum Makunganya na Mwenyekiti wa Mkoa wa Dar es Salaam na mjumbe wa kamati kuu, Joachim Mwakitiga.

Wakizungumza baada ya kukabidhiwa kadi za chama chao kipya jana, viongozi hao walisema UDP imegeuzwa mali ya mtu mmoja ambaye huamua mustakabali wa chama kwa matakwa yake. 
 
Mwakitiga alisema uhai wa chama ni mikutano ambayo inawapa fursa viongozi kujadili na kupanga mikakati ya kukijenga.

Alisema jambo la kushangaza kwenye chama hicho mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, John Cheyo haitishi mikutano wala vikao vya ndani. 

Makunganya alidai kwa miaka mitano chama hicho hakijaitisha mikutano wala vikao vya kamati kuu na halmashauri kuu ya chama.

 Alisema chama ni taasisi na taasisi ni watu, hivyo, viongozi waanzilishi wanatakiwa kufahamu kwamba chama siyo mali yao bali ni ya wanachama wote. 

Makunganya alisema amejiondoa katika chama hicho ili kutafuta demokrasia ya kweli sehemu nyingine.

Katibu Mkuu wa CCK, Renatus Muabhi alisema wameanza operesheni ya kukijenga chama chao na viongozi wataanza kuzunguka nchi nzima kufungua matawi na kuchagua viongozi.
Share:
Weka Maoni yako Hapa

Habari Zinginezo:

0 comments:

Post a Comment

Become a Fan

Popular Posts

Copyright © 2025 GUMZO LA JIJI | Powered by Blogger