Tuesday, July 21, 2015

Uandikishaji BVR Dar kuanza kesho


 Uandikishaji wa wapigakura kwa kutumia Biometric Voters Registration (BVR) Dar es Salaam, unaanza rasmi kesho, huku mashine zaidi ya 4,000 zikitarajia kutumika kukamilisha kazi hiyo katika vituo 1,700.

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji mstaafu Damian Lubuva alisema tume ina imani uandikishaji utafanyika kwa utulivu na amani.
“Mkoa wa Dar es Salaam umepata bahati, kwani tunatarajia kuwa na vifaa vya kutosha,” alisema Lubuva na kuongeza:
“Kuna vifaa vingi vinarejeshwa kutoka mikoani, tunatarajia vitatumika vizuri hapa.”  Alisema NEC tayari imekutana na wadau wakiwamo viongozi wa ngazi mbalimbali na kuwataka  kuhamasisha watu kujitokeza kujiandikisha. 
Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Takwimu la Taifa (NBS) za makadirio ya watu wenye sifa ya kupiga kura, zinaonyesha kuwa Dar es Salaam ina zaidi ya watu milioni 2.9, idadi ambayo ni sawa na jumla ya wapigakura katika mikoa sita ya Katavi, Lindi, Shinyanga, Njombe, Iringa na Rukwa.
Awali, NEC ilitangaza kuahirishwa tarehe ya kuanza uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani hadi hapo itakapotangaza tena.
Mkurugenzi wa Uchaguzi, Julius Mallaba alisema hatua hiyo ilitokana na kuchelewa kuwasili kwa vifaa vya kuandikishia wapigakura.
Uandikishaji katika Mkoa wa Dar es Salaam ulitarajiwa kuanza Julai 4 mwaka huu, lakini ukasogezwa mbele hadi Julai 16, tarehe ambayo nayo ilisogezwa mbele ili kutoa fursa kwa wananchi kusherekea Sikukuu ya Eid el Fitr.
Share:
Weka Maoni yako Hapa

0 comments:

Post a Comment

Become a Fan

Popular Posts

Copyright © GUMZO LA JIJI | Powered by Blogger